Monday, September 12, 2011

Aguero: Ajipanga kuwa Maradona wa City


Sergio Aguero anaonekana kuwa mchezaji muhimu ndani ya Manchester City, umuhimu kama aliokuwa nao Diego Maradona wakati alipokuwa anaichezea Napoli.

Aguero, ambaye amemuoa mtoto wa Maradona, amefunga magoli sita kwenye mechi nne alizoichezea City, toka ajiunge nayo kwa dau la £38 ml alipotokea timu ya Atletico Madrid, kwenye kipindi cha majira ya joto.

Na anapewa nafasi kubwa ya kuiongoza na kuiwezesha City kwenye ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza, kama ambavyo Maradona alifanya akiwa na Napoli.

Maradona aliiwezesha timu hiyo ya Italia kushinda Serie A mara mbili, Kombe la UEFA na Coppa Italia, wakati mchezaji huyo toka Argentina alipokuwa kwenye hiyo timu.

"Naamini ntaweza kuisaidia Manchester City kufanya mambo makubwa kama Diego alivyofanya akiwa na Napoli," Aguero alisema.

"Nimekuja hapa kuisaidia timu kukua na iweze kushinda makombe, na kama tukifanya hivyo mwaka huu itakuwa ni vizuri sana,. Ila tutajitahidi kuwa wazuri zaidi na nategemea kutoa mchango mkubwa  kwenye hilo."

Evra: Lazma tuwe makini

  
Patrice Evra amewaasa wachezaji wenzake wa Manchester United, kuwa makini na kuendelea kukaza buti baada ya kuanza msimu mpya wa ligi kwa rekodi nzuri.

"Tunafanya na inaonekana kama rahisi, lakini si kweli." Alisema alipokuwa anaongea na gazeti la The Independent, "Ninawaheshimu sana Manchester City - wana kikosi makini sana."

"Walipoifunga Tottenham 5-1, tuliiangalia mechi na tukasema ni vyema tukacheza vizuri tukikutana na Arsenal - na tukafanikiwa kushinda kwa goli nane."

"Inaonekana kama ni mashindano kati ya timu hizi mbili, ila msisahaua Chelsea na Liverpool. Japokuwa, kila niwaonapo watu kitu cha kwanza kwao kuuliza ni tarehe ya mechi na wapinzani wetu."

Viingilio Mechi za Chamazi

Timu za Simba na Yanga zitaanza kuutumia Uwanja wa Azam Chamazi ulioko Mbande, Dar es Salaam wiki hii. Septemba 14 mwaka huu Simba itakuwa mwenyeji wa Polisi Dodoma wakati siku inayofuata African Lyon itakuwa mwenyeji wa Yanga.

Kwa mujibu wa msemaji wa Shirikisho hili Boniface Wambura, Viingilio kwa mechi zinazohusisha timu za Yanga na Simba kwenye uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua mashabiki 7,000 tu vitakuwa sh. 15,000 kwa jukwaa kuu na sh. 5,000 mzunguko.

Kwa timu nyingine za Dar es Salaam zinazotumia uwanja huo kiingilio kitaendelea kuwa kile kile cha sh. 10,000 jukwaa kuu na sh. 3,000 mzunguko.

Simba na Azam zaingiza Ml. 72


Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Azam na Simba iliyochezwa Septemba 11 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 72,167,000.

Kwa mujibu wa msemaji wa Shirikisho hili Boniface Wambura, Watazamaji waliokata tiketi kwa ajili ya kushuhudia mechi hiyo walikuwa 21,129. Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa sh. 15,000, sh. 7,000, sh. 5,000 na sh. 3,000.

Viti vya bluu na kijani ambavyo kiingilio kilikuwa sh. 3,000 viliingiza watazamaji 18,586, hivyo kuingiza sh. 55,758,000.

Marekebisho Mechi za Uwanja wa Taifa

Ili kutekeleza maagizo ya Serikali kucheza mechi mbili tu za Ligi Kuu ya Vodacom kwenye Uwanja wa Taifa, Shirikisho la Soka Nchini (TFF) limefanya marekebisho kwa baadhi ya mechi zilizokuwa zichezwe kwenye uwanja huo.

Kwa mujibu wa msemaji wa Shirikisho hili Boniface Wambura sasa, mechi zitakazochezwa Uwanja wa Taifa ni – mechi namba 39- Azam vs Yanga (Septemba 18), mechi namba 50- Simba vs Mtibwa Sugar (Septemba 25), mechi namba 52- Yanga vs Coastal Union (Septemba 28) na mechi namba 58- Yanga vs Kagera Sugar (Oktoba 13).

Nyingine ni mechi namba 62- Simba vs African Lyon (Oktoba 16), mechi namba 65- Yanga vs Toto Africans (Oktoba 20), mechi namba 72- Simba vs JKT Ruvu (Oktoba 22), mechi namba 78- Yanga vs Simba (Oktoba 29) na mechi namba 86- Moro United vs Simba (Novemba 2).

Mechi zifuatazo zitachezwa Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam; mechi namba 35- Simba vs Polisi Dodoma (Septemba 14), mechi namba 29- African Lyon v Yanga (Septemba 15), mechi namba 45- Yanga vs Villa Squad (Septemba 21), mechi namba 66- Simba vs Ruvu Shooting (Oktoba 19) na mechi namba 71- Yanga vs Oljoro JKT (Oktoba 23).

Mapato Mechi ya Yanga na Ruvu Shooting


Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Yanga na Ruvu Shooting iliyochezwa Septemba 10 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 23,388,000.

Kwa mujubu wa taarifa iliyotumwa kwa Yyombo vya Habari na Ofisa Habari na Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Boniface Wambura, inasema  Watazamaji waliokata tiketi kwa ajili ya kushuhudia mechi hiyo walikuwa 6,566. Viingilio vilikuwa sh. 15,000, sh. 7,000, sh. 5,000 na sh. 3,000.